Wananchi
wa mkoa wa Shinyanga wameelezea kufurahishwa kwao na huduma za matibabu
zinazotolewa na madaktari bingwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa huo.
Wakizungumza
na mwandishi wetu aliyetembelea katika hospitali hiyo, mmoja wa wazee
waliopata huduma ya matibabu ya ugonjwa wa moyo Bi. Salu Shinge amesema
amekuwa akisumbuliwa na maumivu ya moyo kwa muda mrefu lakini baada ya
kuonana na Daktari bingwa siku ya Jumatatu na kuanza kutumia dawa, hali
yake imbadilika na kwamba anajisikia nafuu kwa sasa.
"
juzi nilikuwa naumwa sana, nilikuja hapa mwili ukiwa umevimba,
nikamwona daktari akanipa dawa za siku tano, leo ni siku ya tatu, tayari
nimeona mabadiliko makubwa. Nina imani nitapona, nawashukuru sana hawa
waliotuletea madaktari."
Naye
mama wa mtoto Faida Sayi amesema mtoto wake aliyekuwa anasumbuliwa na
uvimbe shingoni kwa muda mrefu amepata huduma ya upasuaji na hivi sasa
anaendelea vizuri.
"Uvimbe
ulianza kama jipu lakini siku zilivyozidi kupita uvimbe haukuwa na
usaha wowote kama ilivyo kawaida ya majipu. Tumehangaika na matibabu
hadi kwa waganga hatukufanikiwa. Niliposikia kuna madaktari bingwa hapa
nikamleta, wamempasua, saa anaendelea vizuri tu".
Hadi
sasa jumla ya wagonjwa 450 wamepatiwa huduma za matibabu, ambao kati
yao wagonjwa SABA wamefanyiwa upasuaji, wakiwemo watoto WATATU.
Huduma
hizo za matibabu zitatolewa hospitalini hapo kwa muda wa siku tano
kuanzia Jumatatu hadi Ijumaa kwa ushirikiano wa Mfuko wa Taifa wa Bima
ya Afya na madaktari bingwa kutoka Hospitali ya Taifa Muhimbili.
Wananchi
wakisubiri kujiandikisha kwa ajili ya kupata namba za kuwaona madaktari
bingwa wanaoendelea kutoa huduma katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa
Shinyanga.
Wananchi wakisubiri kuingia kwenye vyumba vya madaktari bingwa ili kupatiwa huduma.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...