Balozi wa Star Times ambae pia ni mchambuzi wa soka Shafii Dauda akizungumza na waandishi wa habari jana kuhusiana na ushiriki wa king'amuzi hicho katika kuendeleza soka nchini, hiyo ilikuwa ni wakati wa maadhimisho ya wiki yahuduma kwa wateja pembeni yake ni Meneja wa Operesheni wa Star Times Gaspa Ngowi.
KATIKA kuadhimisha wiki ya huduma kwa wateja inayosherehekewa
na taasisi pamoja na makampuni mengineyo duniani kote, kampuni inayotoa huduma
za matangazo ya luninga kwa dijitali nchini ya StarTimes imesema kuwa imepiga
hatua kubwa katika maboresho ya huduma zake.
Akizungumza na waandishi wa habari mwishoni mwa wiki, Makamu
wa Rais wa StarTimes Tanzania, Bi. Zuhura Hanif amebainisha kuwa wiki hii hutoa
fursa ya kipekee ya kupima huduma wanazozitoa kwa wateja na namna ya kuzifanyia
maboresho.
“Tunapokutana na wateja wetu ana kwa ana ndivyo hutuwia
urahisi kwetu kuweza kujua wanahitaji nini hasa. Ukizingatia ndani ya wiki hii
yote wateja wetu wamehudumiwa na wakuu wa vitengo mbalimbali. Kwa mfano kwa
sasa tunafanya jitihada nyingi za kusambaza huduma zetu mikoani ili kuwafikia
wateja wengi zaidi wa vijijini.” Alisema Bi. Hanif
Amesema kuwa mpaka hivi sasa Kampuni yake imekwishaifikia
mikoa takribani 18 nchini Tanzania na mipango ni kusambaza zaidi kila pembe ya
nchi.
“Tunatoa huduma zetu kwa bei nafuu zaidi ili kila mtanzania
aweze kumudu lengo ikiwa ni kila mmojawapo afurahie ulimwengu wa dijitali
nchini.” Alisema.
Kwa upande wake Meneja wa Operesheni wa StarTimes Tanzania,
Bw. Gaspa Ngowi naye amesema kuwa katika kuboresha huduma zao kampuni
imeboresha chaneli za michezo kwa kutambulisha vifurushi vipya mahususi kwa
wapenzi wa michezo nchini.
Meneja huyo ametaja kuwa vifurushi hivyo ni vya Sports Play
na Sports Plus ambavyo amefafanua kuwa ni kama nyongeza ya vifurushi viwili
vilivyopo vya Mambo na Uhuru.
“Hivi sasa wateja wetu wa kifurushi cha Mambo wanaweza
kujiongeza kwa kuongeza malipo kidogo ya Sports Play ambapo wataweza
kujivinjari na ligi za Bundesliga ya
Ujerumani, Serie A ya Italia na Ligue 1 ya Ufaransa ‘Live’ kupitia chaneli za Sports
Arena, Fox Sports na Sports Life.”
Vilevile kwa wateja wa kifurushi cha Uhuru nao wanaweza
kuongezea malipo kidogo kwa ajili ya Sports Plus ligi hizo hizo kupitia chaneli
za Sports Life, Sports Premium na World Football channels.
Bw. Ngowi aliendelea kwa kusema
kuwa machaguo ya vifurushi hivi vipya kunaonyesha kujidhatiti kwa kampuni ya
StarTimes katika maboresho, ubunifu na kuwajali zaidi wateja wake hususani
wapenzi wa soka kuweza kutazama michuano na ligi mbalimbali kwa bei nafuu.
“Siku zote tutabaki kuwa waaminifu
kwa wateja wetu kwa kuwapatia huduma za kipekee kutoka StarTimes kwa
kuwawezesha kufurahia michezo mbalimbali na tena kwa machaguo ya bei
zinazolingana na vipato vyao.” Aliongezea
Bei za kifurushi cha Sports Play
ni shilingi 5000/- na Sports Plus ni shilingi 14,000/- tu.
“Hii inamaanisha kwamba kwa wateja
wa Mambo ambao wanalipa shilingi 12,000/- itabidi waongezee shilingi 5000- ili kupata
kifurushi cha Sports Play na wateja wa Uhuru wanaolipia shilingi 24,000/-
itabidi waobgezee shilingi 14,000/- ya kifurushi cha Sports Plus,” alisema Bw.
Ngowi na Kumalizia, “Kwa kufanya hivyo wataweza kutazama mechi zote Live na pia
kwa wateja wa kifurushi cha Kili kuna ongezeko kidogo la bei kwani wao
watalipia shilingi 48,000/- na kuweza kupata chaneli zote za vifurushi vya
michezo.”
Akitoa maoni juu ya huduma za StarTimes nchini, mtangazaji na
mchambuzi nguli wa masuala ya michezo, Bw. Shaffih Dauda amepongeza sana
jitihada za kampuni hiyo katika kuunga mkono shughuli za michezo hususani soka.
Amesema kuwa kuonyesha uthubutu wao katika kudhamini ligi ya
daraja la kwanza ni tukio linalohitaji pongezo kubwa sana.
“Kwa muda mrefu kilio cha wapenzi na wadau wa soka nchini ni
kupata udhamini kwa ligi ya daraja la kwanza ambayo huibui vipaji vingi zaidi
tunavyoviona ligi kuu. Kwa udhamini huu wa StarTimes tunaamini kuwa utaongeza
hamasa zaidi, utainua ari na pia kufanya ligii hii kuwa yenye ushindani zaidi
ambapo soka la Tanzania litajionea timu nzuri zaidi zikitengenezwa na wachezaji
wazuri zaidi wakipatikana ambao si hazina tu kwa ligi kuu bali pia hata kwa
timu ya taifa na kimataifa.” Alihitimisha Bw. Dauda
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...